Monday, 10 November 2014

MSUVA AMTEGA MAXIMO!

Kiungo mshambuliaji wa Yanga, Simon Msuva.
KIUNGO mshambuliaji wa Yanga, Simon Msuva, amemtega kocha wake Mbrazili, Marcio Maximo kwa kumwambia kuwa ampange kwenye kila mechi ya Ligi Kuu Bara kama anataka ushindi...

Msuva, mwenye kasi ya hali ya juu, aliyetua Yanga akitokea Moro United takribani misimu miwili iliyopita, wikiendi iliyopita aliifungia timu yake mabao mawili katika mechi ya ligi kuu wakati Yanga ilipocheza na Mgambo JKT. Alifunga akitokea benchi kuchukua nafasi ya Haruna Niyonzima.
Kiungo huyo, hana nafasi kwenye kikosi cha kwanza cha Yanga tangu Maximo alipokabidhiwa mikoba ya kukinoa kikosi hicho, badala yake anamtumia kama ‘Super Sub’ kwa ajili ya kubadilisha mchezo na ushindi.
Akizungumza na Championi Jumatatu, Msuva alisema kuwa anaamini ana uwezo mkubwa wa kufunga na kutengeneza mabao kwa wakati mmoja, hivyo anamuomba kocha huyo ampe nafasi ya kucheza katika kikosi cha kwanza.
Msuva alisema, anaamini ushindani upo mkubwa katika timu, lakini hali hiyo haiwezi kumnyima kucheza katika kikosi hicho kwa kuwa anawapita wengi kiuwezo.“Ninaamini ushindani wa namba upo mkubwa kutokana na uwepo wa wachezaji wengi, licha ya ushindani huo uliopo katika timu, ninaamini bado nina nafasi ya kucheza katika kikosi cha kwanza.
“Ukitaka kuthibitisha hilo, mimi mechi zote ambazo nimeingia nikitokea benchi nimekuwa nikibadili matokeo kama sitafunga basi nitatengeneza nafasi ya kufunga mabao kwa wachezaji wengine, hilo halina ubishi.
“Hivyo kocha kama anahitaji ushindi wa mabao mengi katika timu, basi anianzishe kwenye kikosi cha kwanza uone tutakavyofunga, tena ushindi wa mabao mengi,” alisema Msuva.
Baba wa mzazi huyo, Happygod Msuva, aliwahi kulalamika mwanaye kuanzishwa benchi akiwa ana uwezo mkubwa wa kucheza dakika 90 huku akimtaka Maximo kumuanzisha kwenye kikosi cha kwanza.

No comments:

Post a Comment