Wednesday, 29 October 2014

PHIRI APEWA MECHI MBILI SIMBA SC!

 
Kcha mkuu wa Simba Mzambia, Patrick Phiri

 UONGOZI wa Klabu ya Simba chini ya kamati ya utendaji, umelipa benchi la ufundi la kikosi chao mechi mbili za kubadili mwenendo wa matokeo ya timu na kuhakikisha timu inapata ushindi na kucheza mpira unaovutia.
Tangu kuanza kwa Ligi Kuu Bara msimu huu, Simba imekuwa ikipata matokeo yasiyovutia huku ikicheza michezo mitano na kuambulia pointi tano jambo lililoilazimu kamati ya utendaji kukaa na kujadili mwenendo wa timu.
Akizungumza na Championi Jumatano, Katibu Mkuu wa Simba, Stephen Ally, alisema uongozi wa klabu hiyo, ulikaa kikao juzi Jumatatu katika Hoteli ya JB Belmont jijini Dar na kuazimia kuwa benchi la ufundi linaloongozwa na Kocha Mzambia, Patrick Phiri, lipewe mechi mbili na baada ya mechi hizo kamati itakaa na kujadili matokeo yatakayokuwa yamepatikana na pia kuchukua uamuzi juu ya benchi hilo.
Stephen aliongeza kuwa uongozi, umewatekelezea yote walioomba kama benchi ili kuhakikisha timu inafanya vyema katika msimu huu ila kwa mechi tano za awali, bado timu haijaibuka na matokeo yenye kuridhisha.
“Kabla ya msimu kuanza, timu iliweka kambi Zanzibar na ikaendelea kukaa kwa wiki mbili baada ya ligi kuanza na baadaye kuweka tena kambi hapa Dar. Kuna kipindi timu ilienda kambi nchini Afrika Kusini lakini bado haifanyi vizuri, hivyo benchi la ufundi limepewa mechi mbili kubadili mwenendo wa matokeo ya timu,” alisema Ally.
.

No comments:

Post a Comment