

SIKU chache
baada ya straika wa Yanga, Jerry Tegete kuiongoza timu hiyo kuibuka na
ushindi ugenini tangu kuanza kwa michuano ya Ligi Kuu Bara msimu huu
ilipocheza dhidi ya Stand United ya Shinyanga, baba mzazi wa mchezaji
huyo, Mzee John Tegete, ameuvaa uongozi wa klabu hiyo na kuutaka uache
majungu.
Tegete aliifungia Yanga mabao mawili ilipoitandika Stand United mabao
3-0, Jumamosi iliyopita mjini Shinyanga na kuifanya ipande juu katika
msimamo wa ligi hiyo kwa kufikisha pointi kumi.
Nyota huyo ambaye alijiunga na Yanga akitokea Shule ya Sekondari
Makongo, hivi sasa ndiye anayeongoza kwa kuzifumania nyavu klabuni hapo
pamoja na kwamba amecheza dakika 20 tu.
Akizungumza na Championi Jumatano, Mzee Tegete alisema kuwa mwanaye
huyo amewaziba midomo wale wote waliokuwa wakimchukia na kumfanya akose
nafasi katika kikosi cha kwanza cha Yanga licha ya kuwa na uwezo mkubwa
wa kuzifumania nyavu kuliko mchezaji mwingine klabuni hapo kwa hivi
sasa.
Alisema kitendo cha mwanaye huyo kuwa benchi muda mwingi bila ya
kucheza kilikuwa kikimuumiza sana na alikuwa akiwapigia kelele mara kwa
mara viongozi wa Yanga juu ya jambo hilo, lakini waliziba masikio kwa
sababu tu ya chuki binafsi.
“Siku zote nilikuwa nikimwombea mazuri mwanangu juu ya wale
wanaomchukia kwa kila nilipokuwa nikiwauliza kwa nini hachezi,
waliniambia kuwa hachezi kwa sababu anapokuwa uwanjani hufanya mzaha,
jambo ambalo si kweli kabisa, Tegete hayupo hivyo ila yeye ni mtu wa
watu na hupenda kucheka na kutaniana na kila mtu.
“Hata hivyo, pamoja na yote hayo, namshukuru Mungu, mwanangu
ameonyesha kuwa yeye ni bora zaidi katika kikosi cha Yanga hata kama
wanamchukia lakini atabakia kuwa bora,” alisema Mzee Tegete ambaye pia
ni kocha mkuu wa timu ya Toto African ya jijini Mwanza.
No comments:
Post a Comment