
Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Pope.
MWENYEKITI
wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Pope pamoja na wajumbe
wengine wa kamati za klabu hiyo, wamepigwa marufuku na uongozi
kuzungumzia klabu hiyo kwani ni nje ya mamlaka yao na nyadhifa zao.
Hans Pope amekuwa akizungumza katika redio na TV, pia kunukuliwa na
magazeti mara kwa mara juu ya mwenendo wa timu ya Simba huku
akiyazungumzia mambo ya kiuongozi na ya kiutaalam zaidi.Mbali na yeye,
pia viongozi wengine wa Simba wamekuwa wakizungumza mara kwa mara kuhusu
timu hiyo.
Katibu wa Simba, Stephen Ally alisema kuwa kamati ya utendaji ya
klabu ilikaa kikao juzi na kuamua kuwa siyo kila kiongozi ataruhusiwa
kuzungumzia mambo ya klabu bali kamati iliamua jukumu hilo kufanyika na
viongozi wanne tu.
Viongozi wenye mamlaka ya kuizungumzia klabu ni rais, makamu wa rais,
katibu na msemaji wa klabu. Kiongozi mwingine nje ya hao hatakuwa na
mamlaka ya kuifanya kazi hiyo.
Stephen aliongeza, japokuwa Hans Pope amezoeleka katika vyombo vya
habari, tayari wamemtumia taarifa ya kuacha kufanya hivyo na kama
atazungumza basi yawe ni masuala yake binafsi na siyo yahusuyo timu au
klabu kwa jumla.
“Wenye mamlaka ya kuizungumzia klabu kwa ujumla ni watu wanne tu na
siyo kila mwenye cheo Simba ana uwezo wa kutoa kauli juu ya klabu na
ikanukuliwa na wanahabari.Hans Pope tumeshamueleza, mara baada ya kikao
alipewa taarif kuwa hatakiwi kuzungumza kuhusu timu tena.,” alisema
Ally.
Hans Pope ni kiongozi wa muda mrefu sana Simba na alikuwa kwenye timu
hiyo tangu utawala wa aliyekuwa mwenyekiti wa timu hiyo, Ismail Aden
Rage.
Haya yametokea baada ya hivi karibuni wachezaji watatu wa Simba, Amri
Kiemba, Haroun Chanongo na Shaban Kisiga kusimamishwa kutokana na utovu
wa nidhamu na kiwango kibovu, ambapo viongozi mbalimbali wamezungumzia
suala hilo, jambo ambalo limezua maswali mengi.
No comments:
Post a Comment