Monday, 10 November 2014

OKWI AOKOA JAHAZI MSIMBAZI!

Dar es Salaam. Hatimaye Simba imepata furaha baada ya jana kuibuka na ushindi wa kwanza wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu kwa kuichapa Ruvu Shooting Stars bao 1-0 katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam...
Simba ilishuka uwanjani hapo ikiwa na sare sita katika michezo yao sita ya Ligi Kuu iliyocheza msimu huu na ushindi kwao ulikuwa ukisubiriwa kwa hamu na mashabiki wa timu hiyo.
Katika mechi ya jana, bao la Emmanuel Okwi la dakika ya 78 lilitosha kuipa ushindi muhimu Simba ambayo hivi sasa imefikisha pointi tisa kutokana na michezo saba waliyocheza.
Simba ilianza vizuri katika mchezo huo na kutengeneza nafasi kadhaa kipindi cha kwanza kupitia kwa Okwi, ambaye shuti lake lilipaa akiwa ndani ya eneo la hatari pamoja na Amissi Tambwe aliyepiga shuti dhaifu ndani ya hatua sita.
Muda mwingi wa mchezo Simba ilionekana kuhitaji zaidi ushindi kuliko Ruvu Shooting ambao walitumia zaidi utundu wa kupoteza muda na kucheza kwa kushambulia kwa kushtukiza.
Kipindi cha kwanza kilimalizika kwa suluhu huku timu zote zikicheza soka la kiwango cha chini. Kipindi cha pili Okwi, ambaye aliamua kujitoa zaidi katika mchezo huo, alipoteza nafasi ya wazi alipounganisha vibaya mpira uliodondoka nyuma ya mabeki ukitokea wingi ya kulia.
Ukidhaniwa kwamba mpira huo utazaa bao la kuongoza kwa Simba, Okwi aliuunganisha kwa uhakika katika kona ya mwisho ya lango akidhani utakwenda wavuni, lakini ulitoka nje ya nguzo.
Okwi aliyekuwa msumbufu zaidi katika mchezo huo pamoja na Ramadhani Singano, angeweza kupata penalti baada ya kuonekana kama aliangushwa ndani ya eneo la hatari, lakini mwamuzi alisisitiza kuwa alikuwa bado hajaingia na mkwaju wake wa adhabu kudakwa kirahisi na kipa wa Ruvu Shooting, Abdallah Rashid.
Hata hivyo, dakika ya 78, kazi nzuri aliyoianzisha Okwi baada ya kukokota mpira katikati ya mabeki aliimalizia kwa kufunga bao muhimu kwa Simba baada ya shuti la Elius Maguli kupanguliwa na kipa wa Ruvu na hivyo Okwi kuumalizia kirahisi.
Ruvu waliamka baada ya kufungwa bao hilo licha ya mwanzo kuonekana wanahitaji suluhu, lakini umaliziaji wao haukuwa mzuri.
Kwa matokeo hayo, Simba sasa imesogea hadi nafasi ya sita ikiwa sawa na Kagera Sugar yenye pointi tisa pia, lakini ina uwiano mzuri wa mabao. Kabla ya mchezo wa jana, Simba walikuwa katika nafasi ya 11.
Akizungumza baada ya mechi,  kocha wa Simba, Patrick Phiri alisema, “Ushirikiano mzuri kati ya Maguli, Tambwe na Okwi uliisaidia timu yangu kupata ushindi kwa hiyo najisikia furaha.”

No comments:

Post a Comment