Friday, 7 November 2014

MKUDE: JAMANI SIJASAINI SIMBA!

Kiungo wa Simba, Jonas Mkude.
HABARI ni kuwa, Klabu ya Yanga inamhitaji kwa nguvu zote kiungo wa Simba, Jonas Mkude ambaye ili kumshawishi abaki klabuni hapo, uongozi wa Simba ukaamua kumpa gari, lakini mchezaji huyo ametoa kauli nzito...
Mkude ambaye amekabidhiwa gari aina ya Toyota GX 115, ameliambia gazeti hili kuwa, mkataba wake na Simba uliobaki ni ule wa miezi sita pekee na kusisitiza kuwa hajasaini mkataba wowote mpya.
“Kiukweli kabisa mimi bado sijaongeza mkataba mwingine wa kuichezea Simba, ni vema hilo likafahamika kwa watu wote
“Nimebakiza miezi sita ya kuichezea Simba, hivyo hivi sasa naikaribisha timu yoyote kunifuata kwa ajili ya mazungumzo ya awali kunisajili kwa kuwa sheria za soka zinaruhusu.
“Mimi maisha yangu yanategemea soka na kikubwa ninaangalia maslahi,” alisema Mkude kwa kujiamini.
Wakati kiungo huyo akisema hayo, mmoja wa wajumbe wa Kamati ya Usajili ya Yanga ambaye hakutaka jina lake litajwe, aliliambia Championi Ijumaa kuwa, Mkude yupo kwenye mipango ya Yanga kwa ajili ya msimu ujao na ikiwezekana ikawa wakati wa usajili wa dirisha dogo linalofunguliwa wiki ijayo.
“Subiri uone ambacho Yanga watakifanya, nafikiri kufikia Jumamosi (kesho) au Jumapili (keshokutwa) utasikia kitakachotokea kuhusu usajili,” alisema kigogo huyo wa Yanga.Awali, kulikuwa na taarifa kuwa, Simba imempa gari Mkude na kumsainisha mkataba wa miaka miwili ili kuzuia asisajiliwe na Yanga.
“Ukweli wa gari alilopewa Mkude upo hivi, alikuwa akiidai Simba malimbikizo ya fedha tangu utawala wa (Ismail) Rage, alikuwa anadai shilingi milioni sita.
“Kilichotokea ni kuwa viongozi wa sasa wakataka kumlipa, akasema anataka gari katika mazungumzo yake, hivyo walichofanya ni kumuongezea fedha nyingine wakanunua hilo gari,” kilisema chanzo kutoka Simba.
Kuhusu mkataba mpya, chanzo hicho kilieleza kuwa, Mkude alikuwa asaini mkataba tangu timu ikiwa Morogoro katika mechi dhidi ya Mtibwa Sugar wiki iliyopita lakini kukatokea kuchanganyana ratiba ndipo zoezi hilo, halikufanyika.
“Nafikiri atasaini hivi karibuni baada ya uongozi kukaa na Mkude, naona kama vile wamemalizana katika makubaliano, kilichobaki ni kusaini tu,” kiliongeza chanzo hicho.

No comments:

Post a Comment