Friday, 31 October 2014

PHIRI AIGOMEA SIMBA

Kocha wa Simba, Patrick.....
Phiri.
SIKU mbili baada ya kauli ya uongozi wa Simba kuwa umetoa mechi mbili kwa benchi la ufundi kuhakikisha linashinda mechi hizo zote, la sivyo timuatimua itawadia, Kocha wa Simba, Patrick Phiri, amezungumzia juu ya masharti hayo na kuyagomea kimtindo.
Simba imepata matokeo ya sare tano mfululizo katika Ligi Kuu Bara, ndipo Phiri akaliambia gazeti hili kuwa, masharti hayo siyo muhimu kwake kwa kuwa anachotaka siku zote ni ushindi, hivyo suala la kupewa mechi mbili halina nafasi kwake kwa kuwa yeye anapigana ashinde mechi zote na wala siyo mechi mbili alizopewa.
“Sikuja Tanzania kupata ushindi wa mechi mbili pekee, nimesikia kuhusu agizo la mechi mbili lakini kwangu siliweki jambo hilo kichwani. Muhimu zaidi kwangu ni kushinda kila mechi iliyo mbele yangu.“Nafahamu kwamba timu ipo kwenye kipindi kigumu katika kutafuta ushindi, hata mimi pia nimekuwa sijisikii amani katika suala hili.
“Nimekuja Tanzania kwa ajili ya Simba ishinde lakini bado sijafanikiwa,” alisema Phiri na kuongeza:
“Wala sitakuwa na presha ya kuondolewa kwenye timu, kama kutakuwa na hayo mengine tutajua hapo baadaye.”
Wakati hayo yakiendelea, mwenyekiti wa zamani wa Simba, Ismail Aden Rage, ameibuka na kuupinga vikali uongozi wa klabu hiyo kwa kitendo cha kutaka kumfukuza Phiri.
“Hakuna sababu yoyote inayoweza kusababisha uongozi kumfukuza Phiri kwa kipindi hiki, naamini kwa kufanya hivyo timu itazidi kufanya vibaya kwa sababu mbinu zake wachezaji wameshazizoea.
“Naushauri uongozi wa (Evans) Aveva (rais wa Simba), umpe muda kwa kuwa timu ipo kwenye mpito,” alisema Rage na kuongeza:“Unajua Simba walikosea kumtosa yule Mkenya (Donald) Musoti, ni afadhali wangempunguza (Pierre) Kwizera.”

No comments:

Post a Comment