Waandamanaji wakipozi wakati wa vurugu za jana nchini Burkina Faso.
JUMUIA ya Uchumi ya Nchi za Afrika Magharibi (ECOWAS) imetoa onyo kwa
watu wa Burkina Faso kwamba katika vurugu za sasa za kisiasa,
haitatambua hatua yoyote ya kutwaa madaraka kwa njia zisizo za kikatiba.
Hayo yamo katika taarifa iliyosainiwa na Rais wa ECOWAS, John Mahama,
aliyesema jumuia hiyo “imefuatilia kwa wasiwasi mkubwa matukio nchini
Burkina Faso yanayotokana na muswada wa mabadiliko ya katiba.”
Katika vurugu hizo, waandamanji walilichoma bunge la nchi hiyo
wakipinga Rais Blaise Compaore, aliyeiongoza nchi hiyo kwa miaka 27,
kutaka katiba ifanyiwe mabadiliko ili aweze kugombea tena nafasi hiyo
mwaka kesho.
Hata hivyo, bunge la nchi hiyo limesimamisha upigaji kura hiyo ili
kumpa Compaore fursa ya kugombea tena. Kiongozi huyo, alitwaa madaraka
katika mapinduzi ya mwaka 1987 na akashinda katika chaguzi nne
zilizofuata na ambazo matokeo yake yalizua malalamiko.
Mahama alisema ECOWAS imeutambua uamuzi wa serikali wa kuondoa
muswada huo, akisema ni hatua yenye lengo la kuendeleza utulivu na amani
katika nchi hiyo, na amewataka wananchi wa Burkina Faso kuwa watulivu
na kutii sheria, na akayataka majeshi ya usalama kuheshimu katiba ya
nchi.
No comments:
Post a Comment