Friday, 19 December 2014

TAMBWE APIGIWA SIMU ZA VITISHO!


Mshambuliaji Mrundi, Amissi Tambwe.
SIKU chache baada ya kusaini mkataba wa kuitumikia Yanga, mshambuliaji Mrundi, Amissi....
Tambwe, amekuwa akipokea simu nyingi za vitisho kutoka kwa wadau wakimtisha juu ya uamuzi wake huo.
Tambwe alisaini mkataba wa mwaka mmoja Jumatatu iliyopita saa mbili usiku mara baada ya uongozi wa Simba kumkabidhi barua ya kusitisha mkataba wake, muda mfupi kabla ya kufungwa kwa dirisha dogo usiku wa siku hiyo.
Akizungumza na Championi Ijumaa, Tambwe alisema kuwa alianza kupigiwa simu hizo muda mfupi baada ya kutangazwa kuwa anatua Jangwani ambapo wengi waliompigia simu walijitambulisha kuwa ni mashabiki wa Simba na kudai kuwa siyo wote waliomtishia bali wapo wengine waliompongeza.
“Unajua ninawashangaa mashabiki wa Simba hao ambao wananitisha, mimi niliachwa na sikuondoka Simba mwenyewe kama wanavyofanya wachezaji wengine, sasa wananipigia kunitisha ili iweje?
“Wengine wanasema kuwa nitajuta kuichezea Yanga, kitu ambacho siyo sahihi, mimi kazi yangu ni soka, sasa iweje niache kusaini Yanga nikiwa nimekatwa kwenye orodha ya wachezaji watakaoichezea Simba?
“Siyo sawa kabisa, wapo baadhi yao ni waelewa, wenyewe wananipigia na wengine kunitumia SMS za kunitakia kheri baada ya kusaini Yanga na kuniambia maishani popote kwa sababu wanaelewa sijaondoka mwenyewe, viongozi ndiyo walinikata katika usajili wao,” alisema Tambwe kwa masikitiko.
Wakati huohuo, Tambwe na kiungo Pierre Kwizera ambao wote walisitishiwa mikataba yao kuitumikia Simba, wiki hii wanaendelea kusota kufuatilia malipo yao ya kuvunjwa kwa mikataba hiyo huku kukiwa na kauli tata kutoka pande zote mbili.
Akizungumzia juu ya malipo yake ya kuvunjwa kwa mkataba uliokuwa umebakiza miezi sita, kati yake na Simba, jana mchana Tambwe alisema: “Ninataka nimalizane na Simba kila kitu, ili niwe na amani ya kuitumikia Yanga, bado hawajatulipa mimi na Kwizera.”
Naye Kwizera alisema: “Nimeshindwa kurejea nyumbani kwa kuwa bado sijalipwa fedha za kuvunjwa kwa mkataba wangu ambao ulikuwa umebakiza muda wa mwaka mmoja na nusu, niponipo tu kwa sasa naishi Sinza kwa Tambwe.”
Gazeti hili lilipomtafuta Katibu Mkuu wa Simba, Stephene Ally na kumuuliza juu ya suala hilo, jana mchana, alisema: “Tambwe na Kwizera tayari tumemalizana nao kila kitu, ikiwemo barua ya kusitisha mikataba yao na fedha zao wanazoidai Simba.”
Alipoulizwa Ofisa Habari wa Simba, Humphrey Nyasio, alisema: “Wameshalipwa bana, waulize wao vizuri wanajua kila kitu.”Tambwe kwa sasa amehamia Sinza kwa mdogo wake aliyekuwa akiishi naye awali, ametoka Boko ambapo alikuwa akiishi kwenye nyumba aliyopangiwa na Simba.

No comments:

Post a Comment