Monday, 3 November 2014

PHIRI AAMBIWA AANZE KUFUNGA VIRAGO


Kocha Mkuu wa Simba, Patrick Phiri.
UNAKUMBUKA? Uongozi wa Simba ulimpa Kocha Mkuu Patrick Phiri mechi mbili kuhakikisha anapata ushindi vinginevyo kibarua kitaota nyasi lakini tayari ameshaharibu moja, baada ya kutoka sare ya 1-1 na Mtibwa Sugar juzi kwenye Uwanja wa Jamhuri, Morogoro....
Phiri ambaye hajaonja ladha yoyote ya ushindi kwenye ligi msimu huu kikosi chake kikiwa kimetoka sare sita, sasa amebakiza mechi moja tu ya kuhakikisha anasawazisha makosa na mechi yenyewe ni dhidi ya Ruvu Shooting.
Lakini Ruvu Shooting wakijua kwamba Phiri anatakiwa ashinde mechi hiyo itakayopigwa kwenye Uwanja wa Taifa Jumapili ijayo, wamemwambia aanze kukusanya virago.
Akizungumza na Championi Jumatatu, msemaji wa Ruvu Shooting, Masau Bwire, alisema wamejiandaa vya kutosha kuhakikisha wanaibuka na ushindi katika mchezo huo dhidi ya Simba baada ya kuzikosa pointi tatu katika mchezo dhidi ya Coastal Union.
“Tunapenda kumwambia Phiri kuwa aanze kujipanga kwa safari ya kurudi kwao Zambia kwa sababu tumejiandaa vya kutosha kwa ajili ya kuifunga timu hiyo.
“Mchezo huo utakuwa ndiyo wa mwisho kwa Phiri kutokana na kujipanga kwetu, ukichanganya na hasira ya kuzikosa pointi tatu katika mchezo wetu uliopita dhidi ya Coastal,” alisema Bwire.Lakini Phiri mwenyewe amepata kigugumizi kuhusiana na kuelezea kiufundi kinachoisibu timu yake, kwani amedai haelewi kinachoendelea.
Phiri amesema wachezaji wake wamekuwa wakionyesha kiwango kizuri uwanjani lakini hawapati matokeo mazuri.“Nashangaa kwa nini tunapata matokeo ya namna hii, kiukweli wachezaji wangu kama leo wamecheza vizuri sana ingawa wamepoteza nafasi kadhaa, sijui kitu gani kinatokea, kama ni bao tulianza kufunga sisi, ingawa na wapinzani  walikosa penalti,” alisema Phiri.
Simba ipo katika nafasi ya nane kwenye msimamo wa Ligi Kuu Bara ikiwa na pointi sita, baada ya kushuka dimbani mara sita. Ruvu yenyewe ipo nafasi ya saba, ikiwa na pointi saba.

No comments:

Post a Comment