Friday, 7 November 2014

MBUNGE ADAI POSHO KWA WABUNGE ISITISHWE ILI SERIKALI IWEZE KULIPA DENI LA BILIONI 90 ZA (MCD)


Mbunge wa Kisesa kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Luhanga Mpina akizunumza kwenye moja ya vikao vya Bunge mjini Dododma.
WANANCHI wa kada mbalimbali nchini, wamempa ‘big up’ na kumuunga mkono Mbunge wa Kisesa kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Luhanga Mpina (pichani) kwa kitendo chake cha kuomba Bunge la Jamhuri ya Muungano kusitisha mikutano yake, ili fedha zinazolipwa kwa wabunge ziiwezeshe serikali kulipa deni la shilingi bilioni 90 inazodaiwa na Bohari Kuu ya Madawa (MSD) iliyogoma kutoa dawa kwa hospitali za umma...

Wakizungumza kwa nyakati tofauti mara tu baada ya Mpina kutoa kauli hiyo Jumanne wiki hii bungeni Dodoma, wananchi hao wamesema kitendo hicho ni cha kishujaa na kimeonyesha uzalendo wa hali ya juu bila kujali itikadi za kisiasa.
“Hii ni aibu kwa serikali, inashindwa kulipa deni kwa muda mrefu hadi MSD inashindwa kujiendesha, sasa wanapokataa kutoa dawa, maana yake ni maumivu kwa wananchi wa hali ya chini, hasa wa vijijini. Bora wao wa mijini wanaweza kwenda kununua kwenye maduka ya dawa. Serikali haijali kwa sababu vigogo wake wanatibiwa nje kwa hiyo hawaoni umuhimu wa kulipa deni hilo kwa sababu haliwagusi,” alisema Felix Duni aliyejitambulisha kama mjasiriamali, mkazi wa Mbagala, Dar.
John John, mwenyeji wa Nzega mkoani Tabora, alisema hakutegemea kama hoja hiyo ingeweza kutolewa na mbunge wa CCM, kwani kufanya hivyo ni kama kuivua nguo serikali yake, hivyo ujasiri wake unapaswa kuigwa, kwani vikao vya bunge havina umuhimu kuliko afya za wananchi wanaowawakilisha.
“Wao wamechaguliwa na wananchi, katika hali kama hii, lazima waungane kutetea afya zao, serikali lazima itilie maanani suala hili, Bohari Kuu ya Madawa inabebeshwa mzigo wa bure, kwa nini deni linakuwa kubwa kiasi hiki wakati kila mwaka wizara ya afya inapewa pesa? Tunataka wabunge kama hawa wenye kujali wananchi wao,” alisema John alipozungumza kwa njia ya simu.
Gazeti hili lilipokea simu pia kutoka kwa wananchi wa Mikoa ya Singida, Mwanza, Morogoro na Dar es Salaam, ambao walitoa pongezi nyingi kwa mbunge huyo na kumtaka Spika wa Bunge, Anne Makinda kulipa uzito jambo hilo, vinginevyo, waishinikize serikali kulipa deni hilo.
Baada ya mbunge huyo kutoa ombi hilo, Naibu Spika, Job Ndugai alimjibu kuwa suala hilo litapelekwa kwa Kamati ya Uongozi wa Bunge ili kujadiliwa na kwamba jibu lake litatolewa. Hadi gazeti hili linakwenda mtamboni, bado jibu lilikuwa halijatolewa.
Bohari Kuu ya Madawa ilisitisha kutoa huduma kwa baadhi ya hospitali za serikali kutokana na deni kubwa ambalo halijalipwa kwa muda mrefu. Hospitali ya Taifa ya Muhimbili peke yake, inadaiwa kiasi cha shilingi bilioni tisa, kitendo kilichosababisha hospitali hiyo kubwa ya umma kupandisha ada kwa wagonjwa wanaolala na vitanda, jambo ambalo limelalamikiwa sana na wananchi.

No comments:

Post a Comment