
Kijana Sweetbart Joseph (22), mkazi wa
Mbezi Salasala jijini Dar es Salaam, analia na kuhangaika huku akiwa
kitandani kwa miaka nane sasa kutokana na mguu wake wa kushoto kuwa na
uvimbe mkubwa unaomfanya ashindwe kutembea.
CHANZO CHA TATIZO
Akizungumza na waandishi wa
habari hii nyumbani kwao Mbezi Salasala, Sweetbart alikuwa na haya ya
kusema:“Nilianza kuteseka tangu mwaka 2005, nikiwa darasa la sita ambapo
mguu wangu ulianza kuvimba kidogokidogo mpaka nikawa nashindwa kuvaa
kiatu. Ilibidi kiatu cha mguu huo nikipeleke kwa fundi ili kukiongezea
ukubwa.
“Nilimaliza elimu ya msingi kwa shida na nilipojiunga na kidato cha
kwanza nilisoma kwa shida kutokana na kusumbuliwa na mguu huu ambao
umevimba. “Kuna kipindi nilipata homa kali kutokana na kusumbuliwa na
mguu huu ambao ulikuwa ukinifanya nione kama ni jipu kubwa na
kusababisha niwe nakwenda Hospitali ya Temeke kutibiwa.
AFANYIWA UPASUAJI USAHA LITA TATU WATOKA
“Siku
ya kwanza nilipokwenda Hospitali ya Temeke waliamua kunipasua wakatoa
lita tatu za usaha. Walinisafisha kisha wakaniruhusu nirudi nyumbani.
“Nikiwa nyumbani nilipata nafuu, lakini sikuweza kukaa muda mrefu
mguu ukaanza kuuma. Maumivu niliyopata nashindwa namna ya kuyaelezea,
nikawa mtu wa kulia tu!
Kutokana na hali hiyo nikawa nakosa usingizi, wenzangu wakiwa wamelala mimi nikawa nakesha macho.
“Hali yangu ilipozidi kuwa mbaya nilipelekwa tena Hospitali ya Temeke,
daktari mmoja aliamua nilazwe kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi ili
kubaini kilichosababisha mguu wangu kuvimba,” alisema kijana huyo.
Akiendelea kuzungumza alisema kuwa kutokana na mguu wake huo
kumsumbua hata kusoma alikuwa anasoma kwa shida sana japokuwa alikuwa na
uwezo kimasomo darasani.“Ilibidi baadaye nikae tu nyumbani huku
nikiugua mguu ndipo wazee wangu wakaamua kubadili sehemu ya kutibiwa,
kama siyo mguu huu nina hakika ningekuwa nasoma chuo kikuu,” alifafanua
kijana huyo huku akionekana mwenye huzuni.
KUHAMIA MUHIMBILI
“Nilikwenda Hospitali ya Taifa
ya Muhimbili ambako walinipokea na kunifanyia vipimo vyote hadi vya
kansa na mwisho walinishauri nikatibiwe nje ya nchi.“Baada ya kuambiwa
natakiwa kwenda kutibiwa nje, kuna mtu mmoja alimtafuta daktari wa
nchini India akamweleza tatizo langu akamwambia anaweza kunitibu na
kupona kwa gharama ya shilingi milioni sita.
NALIA KILA SIKU
“Baada ya kuambiwa gharama hiyo
nililia sana kwani familia yangu haina uwezo huo, nikajua kilicho mbele
yangu ni kifo kwa sababu ya kukosa kiasi hicho cha fedha ili nikatibiwe
nchini India,” alisema kijana huyo huku akifuta machozi yaliyokuwa
yakimtiririka.
Ilibidi waandishi wetu wakae kwa dakika kadhaa huku wakimpa pole kwa
tatizo alilokuwa nalo, baada ya kupangusa machozi akaendelea
kusema:“Nalia kwa sababu maisha yangu ni duni na wazee wangu hawana
uwezo wa kunipeleka kutibiwa nje ya nchi kwa gharama ya shilingi milioni
sita nilizoambiwa.
“Kutokana na kushindwa huko, naendelea kuteseka huku nikiwa
kitandani, sijui nitaponaje maradhi haya ambayo yananitesa mwaka wa nane
sasa.Naamini kama nisingekuwa naumwa hivi sasa ningekuwa na hatua kubwa
kimasomo na mambo mengine lakini ndiyo hivyo, nimekuwa mtu wa kulala
ndani tu huku nikipata maumivu makali kila kukicha.
KILIO KWA WATANZANIA
“Nawaomba Watanzania wenzangu waliosoma habari yangu wanisaidie
chochote walichonacho kwani naamini kama nitapata fedha hizo na kwenda
kutibiwa India nitapona na kuwa mtu mwenye furaha na amani kama wengine.
“Yeyote aliyeguswa na mateso yangu anaweza kunisaidia chochote
atakachobarikiwa kwa kutumia namba 0713 739253, ” alisema Sweetbart.
Bila shaka baada ya kusoma habari hii ya kijana Sweetbart umegundua
ni kwa kiasi gani anahitaji msaada wako wa hali na mali, kama umeguswa
na unapenda kumsaidia tumia namba yake iliyopo hapo juu.Shime
Watanzania, kutoa ni moyo na siyo utajiri na Mungu atakupa baraka zake-
Mhariri.
No comments:
Post a Comment